Taarifa kuhusu Daraja la Nyerere, Kigamboni


Kwa muda mrefu nimekuwa nikipokea malalamiko ya wananchi kuhusiana na huduma isiyoridhisha kwenye Daraja la Nyerere linalounganisha Kigamboni na Kurasini.

Malalamiko ya wananchi yako kwenye maeneo makuu matatu:
1. Kutumika kwa madirisha machache ya kukatia tiketi. Daraja la Nyerere lina madirisha 14 ( Saba wakati wa kuingia na Saba wakati wa kutokea). Madirisha yanayotumika ni machache na hivyo kusababisha foleni isiyo na msingi.
2. Tozo za Daraja la Nyerere zipo juu sana hususan kwa magari ya abiria. Hali hii imepelekea Kigamboni kukosa ruti ndefu za kuelekea maeneo mengine ya Jiji la Dar Es Salaam. Gari la abiria linatozwa kati ya Tsh 5000-7000 kwa kila safari ambayo ni gharama kubwa sana kwa kutwa.
3. Kutokamilika kwa kipande kilichobaki toka Darajani hadi kwa Msomali.

Kama Mbunge wa Kigamboni nimekuwa nikifuatilia suala hili kwa karibu sana bila ya mafanikio. Tukumbuke kuwa Daraja la Nyerere lilizinduliwa tarehe 19.04.2016 na sasa ni zaidi ya miezi 9 hamna kinachoendelea na wahusika hawatoi majibu yanayotosheleza.

HATUA NILIZOCHUKUA HADI HIVI SASA

1. Mnamo tarehe 15.06.2016 nilimwandikia barua Waziri wa Ujenzi Mhe. Makame Mbarawa (Mb) kuhusiana na hoja hizi. Pamoja na kufuatilia zaidi ya mara kumi kwa simu, maongezi ya ana kwa ana na meseji, barua yangu haijajibiwa hadi hivi sasa (Angalia kiambatanisho).

2. Vile vile nilikutana na Mkurugenzi wa NSSF Prog Godius Kahyarara tarehe 3.10.2016 kuhusu hoja tajwa hapo juu. Aliahidi kuchukua hatua za haraka lakini hadi hivi sasa hakuna kilicofanyika.

3. Kwa kuwa usimamizi wa Daraja la Nyerere upo chini ya NSSF na kipande kilichobaki kitajengwa na NSSF, niliomba kukutana na Waziri anayesimamia taasisi hii. Nilikutana na Mhe. Waziri Jenista Mhagama (Mb) tarehe 3.12.2016 ofisini kwake. Pamoja na maelezo ya mdomo, nilimkabidhi barua ya malalamiko (Angalia kiambatanisho). Mheshimiwa Waziri aliahidi kuchukua hatua za haraka.
Tarehe 13.12.2016 nilipata nakala ya barua aliyoandika Mhe. Waziri Mhagama kwenda kwa Mkurugenzi Mkuu wa NSSF ili kupata maelezo na ufumbuzi wa hoja nilizotoa. Pamoja na kukumbushia Mhe. Waziri Mhagama hajanipatia majibu ya hoja zangu.

Aidha, maelezo niliyopata toka kwa Mkurugenzi wa NSSF wakati Waziri Mkuu anatembelea Kigamboni tarehe 04.01.2017 ni kwamba fedha zinazohitajika kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kipande kilichobaki ni Tsh 24 Bilioni na alinihakikishia kuwa FEDHA HIZO ZIPO. Michoro (design) ya barabara hiyo IMESHAKAMILIKA. Mkandarasi kwa ajili ya kazi hiyo YUPO.

Pamoja na NSSF kuwa na fedha ya ujenzi wa barabara hiyo, mkandarasi aliye tayari na michoro iliyokamilika, kumekuwa na kigugumizi ya lini kazi hii itaanza.
Inasikitisha pia kuona Mawaziri hawajibu barua pamoja na kukumbushwa mara kwa mara.

Kinachoendelea sasa hakuna lugha nyingine ya kuielezea zaidi ya UZEMBE na KUTOWAJIBIKA.

Naleta taarifa hii kwenu wakazi wa Kigamboni ili nanyi mjue kinachoendelea. Ninakusudia kuyapeleka malalamiko yenu kwa mamlaka ya juu zaidi, baada ya mamlaka tajwa hapo juu kushindwa kupata ufumbuzi.

Dkt Faustine Ndugulile Mb
Mbunge
24.01.2017

Posted in Uncategorized | 2 Comments

Kero za kivuko cha Feri. Matatizo na suluhisho


  1. Huduma ya kivuko kati ya Kigamboni na Kivukoni(Ferry) inalalamikiwa sana na wananchi hususan wakazi wa Kigamboni.
    Huduma ya kivuko imekuwa sio ya uhakika, hakuna usalama na pia vyombo hutumia muda mrefu majini kwa safari moja (Safari moja ilitakiwa kutumia dakika 15-20, lakini Safari hiyo kwa sasa inachukua zaidi ya sana moja au zaidi).

Nini chanzo za changamoto hizi:

  1. Uchakavu wa pantoni zilizopo za MV Kigamboni na MV Magogoni. Pantoni hizi hazijafanyiwa matengenezo makubwa kwa muda mrefu sasa. Kila pantoni ina injini nne lakini si zote zinafanya kazi. Miili ya vivuko ina kutu na milango imepinda.
  2. Ufinyu wa maeneo ya kuingia na kutokea kwenye kivuko. Kwa upande wa Kivukoni, barabara ya kutokea na kuingilia kwenye kivuko ni finyu sana, imebanwa na masoko ya samaki, kituo cha mabasi ya DART, kituo cha mabasi ya UDA na Taxi. Vile vile kufungwa kwa Barabara ya Barack Obama  eneo la Ikulu nako kunachangia kuleta msongamano. Kwa upande wa Kigamboni, barabara ya kuingilia na kutokea  kwenye pantoni ni finyu. Magari yanayoingia na kutoka kwenye kivuko yanapishana kwa tabu. Vile vile shughuli za kibiashara, Bajaj na pikipiki navyo vinasababisha msongamano.
  3. Vyumba vya kusubiria abiria ni vidogo sana hususan kwa upande wa Kigamboni. Wananchi wanapata usumbufu mkubwa vipindi vya asubuhi na jioni waendapo na kutoka kazini.
  4. Uwingi wa wasimamizi. Katika kivuko hhiki kuna watumishi wa TEMESA, Askari Polisi, SUMA JKT, Polisi wa Jeshi (Military Police). Kila moja hawa anafanya lake. Wako bize kupitisha “abiria wao na magari yao”. Askari na wasimamizi hawa hupokea fedha na malipo haya hayaingii kwenye mfuko wa Serikali. Utaratibu huu wa wasimamizi wengi unasabisha usumbufu usio na lazima kwa wananchi.
  5. Ukataji wa tiketi sio mzuri. Kuna na msongamano mkubwa hususan wakati wa asubuhi.
  6. Morali ipo chini kwa watumishi wa TEMESA. Uongozi wa juu wa TEMESA hauwajali watumishi wake. Wanalalamika sana. Zaidi ya 80% ya watumishi wa huduma za kivuko wana mikataba ya muda mfupi ya kati ya 1-3. Nahodha mwenye dhamana ya kuendesha chombo analipwa Tsh 350,000 kwa mwezi na wanafanya shift ndefu hadi  masaa 12 kwa siku. Hali hii imepelekea kwa huduma hii kuhujumiwa. Hujuma ni pamoja na watumishi kwa makusudi kukamisha vivuko mchangani, kuendesha vivuko kwa injini mbili badala ya nne, kuchelewesha safari na kuuza mafuta kwa wavuvi
  7. Uongozi wa TEMESA kushindwa kuwajibika na kusimamia majukumu yake kikamilifu. Wameshindwa kuboresha huduma za kivuko. Wameshindwa kusimamia matengenezo ya vivuko. Wameshindwa kusimamia maslahi ya watumishi. Wameshindwa kusimamia mapato (takribani ya Tsh 5 milioni inapotea kila siku).

Nini kifanyike?

  1. Kuwepo na mpango mahsusi wa kufanya matengenezo ya vivuko hivi. Matengenezo yaanze baada ya daraja la Kigamboni kufunguliwa. Aidha, kitafuywe  kivuko cha muda kuziba pengo la kivuko kitakachopelekwa matengenezo. Vile vile, ununuzi wa pantoni mpya uharakishwe.
  2. Upanuzi wa miundombinu ya Barabara za kuingia na kutokea kwenye kivuko unahitajika. Hili liende sambamba na upanuzi wa sehemu za kusubiria abiria.
  3. Kwa kipindi cha mpito mabasi ya UDA yatumie vituo na barabara za UDART. Pindi mradi wa DART utakapoanza, mabasi ya UDA yahamishiwe kabisa pale Kivukoni na kupelekwa sehemu nyingine ambako hakuna mfumo wa DART.
  4. Mfumo wa kukata tiketi na kuingia kwenye kivuko uwe wa kielektroniki. Kuwe na tiketi za siku na za msimu. Kuna watu wanavuka kila siku, kwa nini awe anakata tiketi kila siku? Kwa nini kusiwe na tiketi wiki au mwezi?
  5. Mfumo wa usimamizi kwenye kivuko unahitaji kuangaliwa upya. Walinzi wa TEMESA, SUMA JKT, Polisi na MP wa Jeshi wote wanafanya kazi gani? Kwa maslahi ya nani? Hawa ndio wanasababisha kero na ndio mwanya wa upotevu wa mapato.
  6. Maslahi na mikataba ya watumishi wa TEMESA iangaliwe upya. TEMESA nayo inahitaji kujipanga upya baada ya mabadiliko ya uongozi hivi karibuni.

Tunashukuru kwa hatua zilichokuliwa na Waziri Makame Mbarawa kwa kubadilisha uongozi wa TEMESA. Tunashukuru pia kwa Mhe. Rais John Pombe Magufuli kwa kufanya ziara ya kushtukiza. Naamini kilio chetu kimefika na mapendekezo haya  yatafanyiwa kazi. Wananchi wanataka kuona huduma ya kivuko iliyo bora, salama na ya uhakika.

Posted in Uncategorized | Tagged , , , | 5 Comments

Tatizo la msongamano. Nini kifanyike?


Kwa mujibu wa Sheria namba 5 ya mwaka iliyoanzisha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imeainisha moja ya majukumu ya taasisi hii ni kuwa hospitali ya rufaa ya Taifa.

Taasisi hii ina uwezo wa kulaza wagonjwa 1500 (bed capacity).  Takwimu zilizopo kwenye tovuti ya taasisi hii zinaonyesha kuwa hospitali hii inapokea wagonjwa wa nje (outpatients) wapatao 1000-2000 kwa siku na wanalaza wagonjwa 1000-1200 (inpatients) kwa wiki.

Kwa muda mrefu tumeshuhudia hospitali hii kuzidiwa na wagonjwa. Wagonjwa wengi wakiwa ni wagonjwa ambayo wangeweza kutibiwa kwenye hospitali za pembezoni. Hali ambayo imesababisha msongamano na baadhi ya wagonjwa kulala chini.

Kumekuwa na kauli kuwa msongamano wa Muhimbili unatokana na huduma za afya zinazotolewa kuwa nzuri. Hoja hii sio sahihi sana. Tatizo la msongamano katika hospitali ya Muhimbili ni la kimfumo. Pamoja na juhudi za Mhe. Rais la kutaka kuondokana na wagonjwa kulazwa chini, bado ongezeko la vitanda halitaondoa matatizo ya msingi. Vitanda vitajaa na bado mahitaji ya vitanda vya ziada yataendelea kuwepo.

Matatizo ya kimfumo ya msongamano ni yapi?

  1. Mfumo wa rufaa in dhaifu. Hospitali ya Muhimbili ilipaswa kupokea wagonjwa ambao wameonwa kwenye hospitali za pembezoni na ambao wanahitaji vipimo au matibabu mahsusi ambayo hayapatikani kwenye hospitali hizo. Kinyume chake, wagonjwa wenye magonjwa ya kawaida ambayo yangeweza kutibiwa pembezoni na kina mama wenye ujauzito usio na matatizo ndio waliojaa Muhimbili. “Chujio” la kuwachuja wagonjwa halipo. Kwa mfano, kuna vituo vya Afya vya Mnazi Mmoja, Ilala na Round Table, Mbagala ambazo zina huduma za msingi za uzazi lakini havitumiki kikamilifu badala wagonjwa wake kupelekwa Muhimbili.
  2. Hospitali na vituo vya Afya vya pembezoni kutokuwa na vifaa and wataalamu wa kutosha-Huduma za Amana, Mwananyamala, Temeke, Rangi Tatu na Vijibweni zilipaswa kuwa vyumba vya upasuaji, vyumba vya kuzalia, vifaa na wataalamu kutosha. Hakuna sababu za msingi kwanini mwanamama atoke PembaMnazi, Kivule, Mabwepande au Chamazi akajifungulie Muhimbili. Hata pale ambapo vifaa vipo na madaktari wapo mzigo husukumiwa Muhimbili. Tujiulize not operesheni ngapi za uzazi (Caesarean section) zinazofanyika kwenye hospitali hizi za pembezoni ukilinganisha na Muhimbili? 
  3. Kutokuwepo na mfumo mzuri wa mawasiliano na uratibu kati ya TAMISEMI na Wizara ya Afya. Hospitali ya Muhimbili na za rufaa ziko chini ya Wizara wakati zahanati, vituo vya afya, hospitali za Wilaya na Mkoa ziko chini ya TAMISEMI. Kila Wizara inafanya mambo yake bila kuwa na mawasiliano na uratibu wa pamoja. Tatizo la msongamano linasababishwa na Tamisemi kutowajibika kikamilifu. Idara ya Afya ndani ya TAMISEMI bado ni ndogo sana kuweza kuratibu huduma za afya. Kuna mjadala ndani ya Wizara ya Afya wa kutaka kurudisha hospitali za mikoa Serikali. Kwangu, hili sio suluhisho. Tutibu mfumo na sio kutengeneza mfumo mbadala.

Nini kifanyike?

  1. Mfumo wa rufaa upitiwe upya na kuimarishwa. Kuwe na vigezo vya kumpatia rufaa mgonjwa kwenda Muhimbili.
  2. Hospitali za pembezoni zijengewe uwezo na kupatiwa Vifaa na wataalamu ili waweze kushughulikia wagonjwa na upasuaji usio na “complications”. Jiji la Dar Es Salaam linakuwa kwa kasi sana, Wizara ya Afya na TAMISEMI zianishe maeneo ya kimkakati ya kujenga vituo vya Afya na hospitali. Kwa mfano, Katika Wilaya ya Kinondoni katika njia ya kuelekea Bagamoyo, zaidi ya hospitali binafsi zaa Rabinisia, Massana na hospitali ya Jeshi Lugalo hakuna kituo kikubwa au  hospitali ya umma. Tuangalie huduma za Afya kimkakati.
  3. Mfumo wa mawasiliano na uratibu wa huduma za Afya uboreshwe na kusimamia vizuri.

Hitimisho

Bila ya kuliangalia tatizo la msongamano kimfumo tutamaliza ofisi zote za umma na bado wagonjwa wataendelea kulala chini.  Tuelekeze juhudi zetu katika kurekebisha mfumo na tatizo la msongamano litapungua.

Posted in Uncategorized | Leave a comment

Buriani Mhe. Eugene Mwaiposa MB


Jana na leo si siku nzuri kwangu. Nikiwa njiani kuja Dodoma, nilipata ajali. Namshukuru Mungu niko salama lakini gari imeharibika sana baada ya kugongwa na Lori la aina ya Semi-trailer. Gari lilivutwa kurudi Dar nami niliendelea na safari ya Dodoma.

Nilipofika Dodoma, Mbunge wa kwanza kuonana naye alikuwa Mhe. Eugene Mwaiposa wa Ukonga. Tulikutana kwenye geti la kuingilia mjengoni. Tuliongea na kutaniana kuhusu michakato ya uchaguzi kwenye majimbo yetu.

Baada ya Bunge kuanza jioni alikuja akakaa kwenye kiti changu na kuongea na Mhe. Esther Bulaya. Aliniomba namba za simu za Waziri mmojawapo nikampa na alipohitimisha maongezi yake na Mhe. Bulaya alirudi kitini kwake. Hii ilikuwa kwenye saa kumi na moja jioni. Alionekana mzima na mwenye afya.

Leo asubuhi nikapata taarifa kuwa Mhe. Mwaiposa ametutoka. Nilishtuka sana.

Nitamkumbuka Mhe. Mwaiposa Kwa ushirikiano wake katika Umoja wa Wabunge wa Dar Es Salaam.

Umetangulia Mhe. Mwaiposa, nasi tuko njiani. Kapumzike kwa amani. 

Dkt Faustine Ndugulile MB

Mbunge wa Kigamboni

Posted in Uncategorized | 1 Comment

MREJESHO WA KIKAO CHA MASHAURIANO KUHUSU MPANGO KABAMBE WA UENDELEZAJI WA MJI MPYA WA KIGAMBONI KILICHO FANYIKA KATIKA UKUMBI WA CHUO CHA MWALIMU NYERERE, KIGAMBONI, TAREHE 10.08.2014


Posted in Uncategorized | Leave a comment

Sherehe ya kukabidhi madawati 650 kwa shule za sekondari za kata 12 Tarafa ya Mbagala


20140731-224528-81928359.jpg

20140731-224528-81928818.jpg

20140731-224529-81929269.jpg
1. Mbunge wa Kigamboni,Dk Faustine Ndugulile, akiangalia madawati kabla ya kukabidhi madawati 650 yenye thamani ya Tsh 69 millioni ,makabidhiano yaliyofanyika katika shule ya sekondari Mbagala.
2.MBUNGE wa Kigamboni,Dk Faustine Ndugulile, akikata utepe kuashiria tendo la kukabidhi madawati 650.
3.MBUNGE wa Kigamboni,Dk Faustine Ndugulile, (katikati),akiwa na baadhi ya watendaji wa halmashauri ya manispaa ya Temeke idara ya elimu, mara baada ya kukabidhi madawati 650 kwa shule 12 za sekondari katika tarafa ya Mbagala jijini Dar Es Salaam.

Posted in Uncategorized | Tagged , , , , | Leave a comment

Ujenzi wa miundombinu Zakhem-Kingugi


20140629-120839-43719218.jpg

20140629-120838-43718607.jpg
Barabara isiyo rasmi ya Zakhem-Kingugi ni njia inayotumika na wakazi wengi wanaoishi maeneo ya Kingugi na Kilungule.
Kwa sasa wakazi wenye magari wanaokwenda Kingugi hutumia njia ya mzunguko kupitia Corner Bar.
Ujenzi wa Box Culvert umeanza na Manispaa imetenga zaidi ya Tsh 100million kwa ajili ya kutengeneza barabara hii.
Naushukuru sana uongozi wa Tazama Pipeline kwa ushirikiano walionipa mimi na Manispaa katika kuanisha eneo la kujenga Daraja na barabara. Ikumbukwe kuwa eneo hili ni sehemu ya hifadhi ya kupitisha bomba la mafuta. Lakini kutokana na mahusiano mazuri kati ya Tazama Pipeline na sisi, wamekubali tujenge Daraja hili na barabara ambayo itakuwa ni mkombozi mkubwa kwa wakazi wa Kingugi na Kilungule.

Posted in Uncategorized | Tagged , , , , , | Leave a comment

Mrejesho wa suala la umeme kwa maeneo mbalimbali ya Jimbo la Kigamboni


Siku ya Jumatatu tarehe 23.06.2014 nilifanya mkutano na uongozi wa Tanesco ngazi ya Mkoa wa Temeke na Wilaya ya Kigamboni. Mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na:

  1. Kukatika kwa mara kwa mara kwa umeme 
  2. Umeme mdogo kwa baadhi ya maeneo 
  3. Uunganishaji wa umeme kwa wateja wapya
  4. Miradi mipya ya umeme kwa Jimbo la Kigamboni

1. KUKATIKA KWA MARA KWA UMEME JIMBO LA KIGAMBONI

Umeme unaopatikana kwa wateja wa Jimbo la Kigamboni unatoka sub-station ya Ilala. Umeme huu pia husambazwa kwa maeneo ya Temeke, Mbagala na Mkuranga. Kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji pamoja na uchakavu wa miundombinu, kumekuwa na ukatikaji wa umeme mara kwa mara.

Tanesco walinieleza kuwa hatua ambazo wanachukua kuondoa tatizo hili ni pamoja na maboresho ya miundombinu, kusafisha njia unaopita umeme huo kwa kukata miti na matawi na kujenga sub-station mpya maeneo ya Mbagala. Kukamilika kwa sub-station ya Mbagala utapunguza utegemezi uliopo sasa kwa sub-station ya Ilala. Kazi ya ujenzi wa sub-station mpya unatarajia kukamilika mwezi Disemba mwaka huu.

2. UMEME MDOGO KWA BAADHI YA MAENEO (LOW VOLTAGE)

Kuna baadhi ya maeneo kama vile Kijichi na Magogoni kumekuwa na tatizo la umeme mdogo. Tanesco walinitaarifu kuwa kuna mpango wa kufanya “voltage improvement” kwa kufanya “phase addition” na kuongeza transfoma nyingine mbili maeneo ya Magogoni. Transfoma zipo na ninatarajia kazi hii itaanza hivi karibuni. Kwa upande wa Kijichi, pamoja na “voltage improvement” bado kutakuwa na tatizo. Suluhu ya kudumu itakuwa kukamilika kwa sub-station ya Mbagala.

Tulikubaliana kuwa kazi hii iwe imekamilika ndani ya miezi mitatu ijayo.

3. UMEME KWA WATEJA WAPYA

Nimekuwa nikipokea malalamiko mengi toka kwa wananchi wengi ambao wamekuwa wakisubiri muda mrefu kupata huduma ya umeme. Malalamiko yamekuwa yakitoka Kibada, Gezaulole, Toangoma, Saku, Rufu na Kiponza.

Uongozi wa Tanesco ulinihakikishia kuwa maandalizi yamekamilika kwa ajili ya usambazaji wa umeme kwenye maeneo ya Kibada (blocks 14,15,16,17,18,19,20).  Waliahidi kukamilisha kazi hii ifikapo mwezi Septemba 2014.

Niliwataka ndani ya wiki tatu (3) kunipa mikakati yao ya kuwapatia umeme wananchi walioomba toka maeneo ya Gezaulole, Mbwamaji, Kizani, Mwera, Kibada(blocks zilizobaki), Ponde, Goroka Kalakala, Masaki na  Malela. Uongozi wa Tanesco uliahidi kufanya hivyo kwani miradi hii imeshatengewa Bajeti zake. Pia, Tanesco haina uhaba wa vifaa vya kuunganisha umeme kwa sasa.

4. MIRADI MIPYA YA UMEME JIMBO LA KIGAMBONI 

Uongozi wa Tanesco ulinitaarifu kuwa maombi yangu ya kutaka Kata za Kimbiji na Pemba Mnazi kuingizwa kwenye mradi wa Umeme Vijijini (REA) yamekubaliwa na sasa kata hizi zitaanza kupata huduma ya umeme.

Kama nilivyoeleza hapo juu, umeme wa sasa kwa Jimbo la Kigamboni hutoka Ilala, ujenzi wa Sub-Station ya Mbagala unaendelea na unatarajia kukamilika mwezi Disemba, 2014. Kukamilika kwa kituo kutafanya baadhi ya maeneo ya Jimbo la Kigamboni kujitegemea kwa huduma ya umeme na pia kuondokana kukatika katika mara kwa mara kwa umeme kama ilivyo sasa.

Vile vile Tanesco ipo kwenye mchakato wa kutafuta eneo katika Tarafa ya Kigamboni kwa ajili ya ujenzi wa sub-station mpya. Katika mwaka huu wa fedha hakuna fedha iliyotengwa kwa mradi huu. Lengo ni kuingiza ujenzi wa sub-station kwenye bajeti ijayo.

Aidha, niliwataka uongozi wa Tanesco kufanya maandalizi ya awali kujua gharama za kufikisha umeme katika maeneo ya Mwasonga, kata ya Kisarawe II ili makisio haya yaingizwe bajeti ya mwakani. Tulikubaliana zoezi hili kufanyika ndani ya miezi mitatu.

5. HITIMISHO 

Shirika la Tanesco halina uhaba wa vifaa kwa sasa. Niliwataka Tanesco Kigamboni kuandaa mpango kazi wa usambazaji wa huduma ya umeme kwa wateja wapya  ambayo itanisaidia kufuatilia utendaji kazi wao; kuboresha mawasiliano na mahusiano na wateja pindi umeme unapokatika au pale wateja wanapofika kuuliza kuhusu hatma ya maombi yao. Kwa vile, Tanesco ina uhaba wa vikosi vya kuunganisha umeme kwa wananchi, niliwashauri waangalie uwezekano wa kutumia wakandarasi binafsi (outsourcing) baadhi ya kazi hizi.

Kwa wananchi wa Kibada, Toangoma na Gezaulole kwa maeneo mliyoniletea orodha zenu, ndani ya siku 21 nitawapatia majibu ya lini maeneo yanatarajiwa kufikiwa. Aidha, nashauri maeneo husika kuunda kamati ambazo zinashirikiana nami katika ufuatiliaji.

Nawasilisha

Dkt Faustine Ndugulile (MB)

Mbunge Kigamboni

Posted in Uncategorized | Tagged , , , | Leave a comment

Bunge la Katiba-Mjadala wa Rasimu-Siku ya tatu


Leo mjadala wa rasimu umeendelea. Kwa mujibu wa kanuni, kamati zilitakiwa kujadili sura mbili kwa siku mbili. Pamoja na kuongeza siku, baadhi ya kamati zimemaliza kazi na nyingine zimeshindwa kukamilisha kazi hii ndani ya muda uliopangwa.

Tulitarajia kuwa kesho uwasilishaji wa taarifa za kamati ungefanyika Bungeni, lakini kuna dalili zote kuwa Bunge kesho litahairishwa ili kupisha kamati kumaliza kazi zao.

Sura ya kwanza na ya sita zimebeba muundo wa Serikali. Sura hizi ndizo zenye mvutano mkali. Tukifanikiwa kukubaliana kwenye sura hizi, tunatarajia sura nyingine zinaweza kwenda kwa kasi zaidi.

Uwezekano wa kumaliza kazi ya kujadili rasimu ya katiba hii ni mdogo. Kuna uwezekano mkubwa kwa Bunge la Katiba kuahirishwa ili kupisha Bunge la Bajeti kukaa na kupitia Bajeti ya Serikali. Vile vile kuna uwezekano tukashindwa kuendelea iwapo pande zote za Muungano zitashindwa kupata 2/3 ya kura zinazohitajika kupitisha ibara mbali za Katiba.
Wiki mbili au tatu zijazo zitatoa picha halisi ya mchakato huu.

Tuendelee kuwa pamoja.

Posted in Uncategorized | Tagged , , , , | 2 Comments

Bunge la Katiba- Mjadala wa Rasimu-Siku ya Pili


Leo mjadala wa rasimu ya katiba umeendelea, huku mvutano ukiwa katika muundo wa Muungano na vile vile kwa baadhi ya wajumbe kutaka kupatiwa nakala za hati ya Muungano na ushahidi wa kuridhiwa kwa Muungano upande wa Zanzibar. Hata hivyo, vielelezo hivi havikutolewa.

Mzee Pius Msekwa ambaye alikuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika wakati Muungano naye alipata fursa ya kutembelea baadhi ya kamati na kutoa ushuhuda wa matukio mbali mbali kabla na baada ya Muungano.

Tulitarajia kumaliza kupitia sura ya kwanza na sita kesho, lakini kutokana na kazi kuwa kubwa, kesho tutaendelea na kazi hiyo. Kamati nyingi zipo katika ngazi ya kupiga kura, huku mwelekeo unaonyesha Muungano wa Serikali mbili kupewa nafasi zaidi na kuungwa mkono na wengi.

Kesho tunatarajia kukamilisha kazi ya kujadili sura ya kwanza na sita.

Posted in Uncategorized | Tagged , , , , | Leave a comment