Magazeti ya leo yana habari kuhusu kusimamishwa kwa baadhi ya watendaji waandamizi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kutokana na sakata la kumilikisha eneo la TAZAMA kwa mfanyabiashara binafsi wa mafuta kinyume cha taratibu.
Jimbo la Kigamboni ni eneo ambalo liko karibu na kitvu cha Jiji la Dar Es Salaam, kutokana na sababu hii, eneo hili limekuwa ni kimbilio la watu wengi kwa sasa.
Mnamo mwaka jana kipindi cha Pasaka, wakazi wa kata ya Tungi walishuhudia ujenzi wa uzio uliokuwa unafanyika usiku na mchana chini ya ulinzi wa Jeshi la Polisi. Kwa jitihada za uongozi wa wananchi katika eneo hili ujenzi huo ulisimamishwa.
Sakata hili limekuja kujitokeza tena majuzi baada ya uongozi wa TAZAMA kulalamika kuhusu kuingiliwa eneo lao. Baada ya uchunguzi wa ndani, umeonyesha kuwa waliohusika kupindisha sheria na kumilikisha eneo la TAZAMA kinyume cha sheria kwa mwekezaji walikuwa watendaji waandamizi wa Wizara ya Ardhi.
Sishangai! Kwani watendaji wa Wizara ya Ardhi wamekuwa ni vinara wa migogoro ya ardhi katika Jimbo la Kigamboni.
Si siri, watendaji wa Wizara walimega na kujigawia viwanja vyingi katika Mradi wa viwanja 20,000 katika eneo la Kisota na Kibada. Hadi hivi sasa wauzaji wakubwa wa viwanja maeneo haya ni watendaji wa Wizara ya Ardhi. Hadi hivi sasa Wizara inapata kigugumizi kufanya mapitio (audit) ya zoezi la viwanja 20,000 pamoja na kulipigia kelele sana suala hili.
Watendaji wa Wizara ya Ardhi wakiwa na wawekezaji bandia wamekuwa wakienda moja kwa moja kwa wananchi na kuwatisha, kuwapokonya ardhi yao na kuwamilikisha wawekezaji bandia bila kufuata taratibu na kuwalipa wananchi fidia chini ya viwango vya Serikali.
Hata mradi wa Mji Mpya wa Kigamboni, kuna mapungufu mengi ambayo yanayosabishwa na watendaji wa Wizara kupindisha sheria na kuweka maslahi binafsi mbele.
Natumai Wizara itachukua nafasi hii kujitathmini, kuondoa watumishi ambao si waaminifu na kurejesha heshima na imani kwa wananchi.
Hivi majuzi nyumba zipatazo 34 za wakazi wa eneo la Minondo, Amani Gomvu, Somangila walivunjiwa ili kupisha ujenzi wa nyumba za vyombo vya ‘ulinzi na usalama’. Kwa mujibu wa wananchi hawa walivamiwa saa kumi alfajiri na kuamriwa kutoka nje ya nyumba zao ili kupisha zoezi la ubomoji. Wananchi hawa wanadai hawakupewa notisi kuhusu zoezi la ubomoaji .
Moja ya nyumba 34 zilizobolewa.











