CCM yashinda Igunga

Chama Cha Mapinduzi kimeibuka kidedea katika uchaguzi mdogo huko Igunga. Katika matokeo ya uchaguzi uliofanyika jana na matokeo kutangazwa leo mgombea wa CCM Dkt Dalali Kafumu amepata kura 26,484, mgombea wa CHADEMA Joseph Kashindye amepata kura 23,260 na mgombea wa Leopold Mahona wa CUF amepata kura 2104.

Napenda kuwapongeza wana CCM wenzangu walioshiriki katika uchaguzi huu na kuleta ushindi kwa chama chetu. Aidha, navipongeza vyama vya CHADEMA na CUF kwakuonyesha ukomavu mkubwa wa kisiasa.
Matokeo haya yana maana gani?

  1. Matokeo haya yanaonyesha ushindani umezidi kuongeza. Mchuano kati ya CHADEMA na CCM ulikuwa ni mkali. Hii inamaanisha CHADEMA kama chama kikuu cha upinzani kinazidi kuimarika na umaarufu wa CCM unazidi kupungua.
  2. Katika uchaguzi wa 2010 chama cha CUF kilipata kura 11,000 lakini ndani ya mwaka mmoja umaarufu umeporoka hadi kufikia kura 2104 kwa mgombea yule yule aliyegombea mwaka jana. Ni vyema chama cha CUF kikafanya tathmini ya kina hapa. Je isingekuwa busara kwa CUF kukiachia na kukisapoti chama cha CHADEMA ambacho kilikuwa na nafasi nzuri kwa upande wa upinzani kwenye uchaguzi huu?
  3. Wapiga kura waliojitokeza hawafiki 18,000. Hali hii iliwanufaisha zaidi CCM ambao wana mtandao mkubwa na mpana. Waliopiga kura wengi walikuwa wakinamama na wazee ambao wengi wanaipenda CCM. Ingawa vijana walishiriki kwa wingi kwenye mikutano ya vyama vya upinzani mwisho wa siku hawakushiriki katika kupiga kura. Hii ni changamoto ambayo vyama vyote, vyama vinapaswa kukuna vichwa na kupanga jinsi ya kuhamasisha vijana ambao kwa sasa ni asilimia kati ya 60-70 ya taifa hili ili waweze kushiriki katika chaguzi na kupata viongozi ambao watawafaa.
  4. Miundo ya vyama kwenye majimbo na wilaya. CCM imeweza kushinda kwa sababu ina mtandao mkubwa katika ngazi zote. Ilikuwa ngumu kwa vyama vya upinzani katika kipindi cha muda mfupi kuweza kuwafikia wapigakura wote na kujinadi.
  5. Bado tuna ushabiki mkubwa wa siasa. Ushiriki wa wananchi kwenye mikutano ni mkubwa lakini inapofika wakati wa kupiga kura ushiriki unakuwa mdogo sana.
  6. Vyama vya upinzani vilishindwa kutumia vyema mapungufu ya chama tawala. Kulikuwa na changamoto nyingi zinazokabili CCM na serikali yake lakini kwa bahati mbaya sana upinzani ulishindwa kuzitumia changamoto hizo kwa manufaa yao.

Uchaguzi sasa umekwisha. Huu ni wakati muafaka kwa washindi na washindwa kufanya tathmini ya kina kuhusu uchaguzi ili kupata matokeo mazuri kwenye chaguzi zijazo.

Mungu Ibariki Afrika Mungu Ibariki Tanzania

About Dr Faustine Ndugulile

#Medical Doctor #Microbiologist # Public Health Specialist #Politician #African #Proud Tanzanian
This entry was posted in Uncategorized. Bookmark the permalink.

3 Responses to CCM yashinda Igunga

  1. hongera sana ccm tunaomba sasa ondoa changa moto zilizopo ili kuandaa mazingira mazuri ya 2015

    Like

  2. Congratulation ccm but make sure you combat challenges faced in your party so as to be in a good position in the coming election

    Like

  3. Paul says:

    Chama cha Chadema tishio,kama 2010 hakikuweka mgombea lakini ktk uchaguzi mdogo uliohitimishwa 2.10.2011 na kujizolea kura hizo ni dhahiri 2015 jimbo ni la chadema.

    Like

Leave a comment