Taarifa kwa umma kuhusu mchakato wa Mji Mji Mpya wa Kigamboni

TAARIFA KWA UMMA

YAH: MAZUNGUMZO YA WABUNGE WA MKOA WA DAR ES SALAAM NA WAZIRI MKUU, DODOMA-TAREHE 07.02.2013

Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda jana tarehe 7.2.2013 alifanya kikao na Wabunge wa Mkoa wa Dar Es Salaam na kuhudhuriwa na Waheshimiwa Abasi Zuberi Mtemvu ambaye ni Mwenyekiti wa Wabunge wa Dar es Salaam, Iddi Azzan, Mussa Azzan Zungu, Eugen Mwaiposa, Neema Himid, Mariam Kisangi, Phillipa Mturano, Halima Mdee, Dkt Milton Mahanga, Sophia Simba na Dkt Faustine Ndugulile. Kwa upande wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi iliwakilishwa na Waziri Anna Tibaijuka na Naibu wake Goodluck Ole Medeye. Kikao hiki pamoja na mambo mengine, kilijadili suala la Mji Mpya wa Kigamboni.

Katika kikao hiki  nilielezea kuwa dhana ya Mji Mpya wa Kigamboni ni nzuri, ila mchakato wa kufikia huko unakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ukiukwaji wa sheria unaofanywa na viongozi na watendaji wa Wizara ya Ardhi. Nilitabanaisha kuwa sheria kama sheria ni nzuri na hazina matatizo yoyote, ila utekelezaji wa sheria hizi umekuwa na mapungufu makubwa.

Ikumbukwe kuwa mchakato huu unatawaliwa na sheria tano ikiwa ni pamoja na Sheria ya Utwaaji Ardhi na. 47 ya mwaka 1967; Sheria ya Mipango Miji na. 8 ya 2007; Sheria ya Ardhi no. 4 ya 1999; Sheria ya Wakala wa Serikali ya 1997 na Sheria ya Serikali ya Mitaa na.8 ya 1982.

Pili, ushirikishaji hafifu wa wananchi, viongozi wa Serikali na wawakilishi wa wananchi ikiwa ni pamoja na Mbunge wa eneo husika. Waziri na Watendaji wa Wizara wamekuwa hawafuati sheria na badala yake kumekuwa wakitumia ubabe, nguvu na usiri mkubwa katika utendaji kazi wao. Aidha, wananchi wamekuwa wakitaarifiwa na sio kushirikishwa katika mchakato wa mradi huu. Kuna tofauti kubwa kati ya kutaarifu na kushirikisha.

Aidha, kuongeza eneo la mradi toka ekari takribani 6,000 hadi kufikia ekari 50,000 bila kuwashirikisha wananchi wa maeneo ya Kisarawe II, Kimbiji, Pemba Mnazi na Somangila kumeleta taharuki kwa wananchi wengi wa maeneo haya.

Vile vile, uanzishaji wa Mamlaka ya kusimamia uendelezaji wa Kigamboni, Kigamboni Development Authority (KDA), umeleta mtafaruku mkubwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kuhusu mamlaka na mipaka kati ya KDA na Manispaa, mamlaka ipi itenge bajeti ya kuendeshea kata chini ya Mradi huu na hatma ya Madiwani katika eneo la mradi.

Vile vile, kutokana na usiri mkubwa kwenye mradi huu wananchi wengi hawafahamu lengo la mradi, haki, stahili na hatma yao.

Katika kikao hiki nilitoa mapendekezo yafuatayo:

  1. Kufanya mapitio ya kisheria kuhusu taratibu na vifungu vya sheria vilivyokiukwa.
  2.  Kuandaa Mpango Kazi wa pamoja kwa kushirikiana na viongozi, wawakilishi wa wananchi pamoja Mbunge. Mipango yote iwe wazi kwa wananchi na kukubaliwa na wote.
  3. Viwango vya fidia viwekwe hadharani na kujadiliwa na wananchi na kuridhiwa.
  4. Ushiriki wa wananchi uwekwe wazi. Mtiririko wa manufaa kwa wananchi uwe kama ufuatao:
    1. Wananchi kuendeleza mwenyewe maeneo yao
    2. Wananchi kuingia ubia na wawekezaji katika maeneo yao
    3. Kuondoka eneo la Mradi kwa hiari baada ya kushindwa (4a-b).
  5. Wananchi watakaopisha eneo la mradi wapatie makazi mbadala. Serikali igharamie ujenzi wa makazi mbadala kwa ajili ya wakazi wenye kipato cha chini, kati na juu. Wananchi watakaohamishwa wapewe kipaumbele cha kwanza katika ununuzi wa makazi mbadala.
  6. Uhakiki wa wamiliki wa ardhi na nyumba ufanyike upya ili wale waliojenga baada ya zuio kuisha wapate fursa ya kuongezwa ikiwa ni pamoja maeneo mapya.
  7. Elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi kabla ya mradi kuendelea.
  8. Majibu na makubaliano ya mapendekezo haya yawe kimaandishi.

HITIMISHO

Katika kuhitimisha. Waziri Mkuu alipitia mapendekezo na kusisitiza mambo yafuatayo:

  1. Masuala ya kisheria yaangaliwe kwa lengo la kuainisha mapungufu na maeneo yanayosigana kisheria hususan utendaji kazi wa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke baada ya kuanzishwa kwa mamlaka ya KDA.
  2. Uwepo mfumo mzuri wa ushirikishaji wananchi kuanzia ngazi za mitaa, na kutengeneza mfumo wa mawasiliano na uwakilishi. Aidha aliongeza kuwa ni vyema pia wanaharakati wakawa kwenye kamati hizi. Vile vile kwa kuwa mradi huu ni mkubwa, ni vyema Wabunge wa Dar Es Saalaam hususan wale wa Kigamboni wakashirikishwa kikamilifu katika mchakato mzima na kuwepo mikutano ya mara kwa mara ya mrejesho. Ajenda hii iwe ya kudumu na elimu ya kutosha itolewe kwa wadau wote.
  3. Wizara iainishe namna gani wananchi watafaidika na mradi huu. Aliagiza mapendekezo niliyotoa kuhusu manufaa kwa wanachi yafanyiwe kazi.
  4. Alishauri zoezi la uhakiki na tathmini lifanyike upya.
  5. Alisisitiza kuwa ni muhimu kwa makazi mbadala kwa wale watakaohamishwa kuwa katika  maeneo ya karibu na Kigamboni.
  6. Aliwataka Mawaziri wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kufanyia kazi maagizo haya pamoja na changamoto zilizoainishwa na maelezo au ufafanuzi kuletwa katika kikao kingine kitakachofanyika Dar Es Salaam katika siku za karibuni.
  7. Mwisho, Waziri Mkuu alisisitiza matumizi ya lugha ya staha pamoja na kujenga “Partnership Dialogue” ili mradi uweze kwenda vizuri.

Napenda kuwashukuru Wabunge wa Mkoa wa Dar Es Salaam kwa ushirikiano walioonyesha na kwa michango mizuri katika kikao hiki. Kwa aina ya pekee, ninamshukuru Waziri Mkuu, kwa kuendesha vizuri kikao hiki kwa hekima na busara.

Ninawaomba wananchi wa Kigamboni kuendelea kuwa watulivu, wakati mimi na Wabunge wenzangu wa Dar Es Salaam tukiendelea kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Waziri Mkuu na pia majibu ya hoja zilizotolewa. Mwisho, niwatake Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuendesha mchakato huu kwa mujibu wa sheria, kwa kuzingatia dhana ya utawala bora na kwa taratibu shirikishi.

Dkt Faustine Ndugulile (MB)

JIMBO LA KIGAMBONI

About Dr Faustine Ndugulile

#Medical Doctor #Microbiologist # Public Health Specialist #Politician #African #Proud Tanzanian
This entry was posted in Uncategorized and tagged , , . Bookmark the permalink.

17 Responses to Taarifa kwa umma kuhusu mchakato wa Mji Mji Mpya wa Kigamboni

  1. Clement Marandu says:

    Well done our MP, tupo pamoja

    Like

  2. eddobat mwanaharakati says:

    Utu wa binadamu kwanza maslahi baadae.Mamlaka ya kigamboni waachiwe wenye kigamboni yao

    Like

  3. ladislaus samson mude says:

    Mwenye haki apewe haki yake,maswala ya mnyonge mnyongeni alafu haki yake ndio ifuatwe hapa sio nina shukuru sana (MB),kwa kulisimamia hili.nami nipo pamoja nawe,tunaipenda ile njia ya asali na maziwa aliyo sema mungu kwenye vitabu vyake

    Like

  4. mheziwa bundala says:

    Sawa kaka ,kaza buti songambele

    Like

  5. Dr. Nhigula says:

    Faustine,
    Mimi ninaona omba mkutano na waziri mkuu na waziri wa ardhi uombe wasifu wa watendaji wote kutoka wizara ya ardhi hii kuona tatizo lipo wapi. Shauri waziri wasifu wao wawasilishe mbele ya waziri mkuu na uonyeshe una wasi wasi labda kuna mapungufu ya kiwango cha kuelewa umuhimu wa mradi kwa watendaji wa wakuu wa huu mradi. Swala linalojitokeza kwa sasa hapa hawataki mbunge ajuwe kuna nini kinaendelea na hii inaonyesha mapungufu ya kielimu…..

    Like

  6. twakushukuru sana mbunge wetu tupiganie mji wetu wa kigamboni ili kila mtu apate haki yake salama bila yakupunjwa kwa maana baadhi ya viongozi wetu wanataka kutuzurumu haki zetu naomba utusaidie usituache tuangamie wew ndie kiongozi wetu tunaekutegemea usituangushe

    Like

  7. franco Mwakatage says:

    Vizuuri mbunge wetu wananchi wa kigamboni tupo nyuma yako tutakufuata popoote utakapokuwa

    Like

  8. DAVIES RWECHUNGURA says:

    ASANTE KIONGOZI JIMBO LA KIGAMBONI LINA MATATIZO MENGI.TEMBELEA HATA MPONDA TUNAKUSUBIRI KWA HAMU

    Like

  9. Honghera mbunge jambo kubwa ni kuzuia vikamati vinavyoudwa na wizara hasa katika mitaa mitatu ya Tungi Uvumba na kifurukwe utatusaidiaje Mheshimiwa mbunge wetu mpendwa.Tafadhali sasa chukua jukumu la mstari wa mbele wa mjuhudi za kusaidia umma wa wanyonge ambao sasa haki zao zitapotea.

    Like

  10. muheshimiwa mbunge wetu mimi ni mwana kifurukwe kilichopo huku ni kwamba diwani na mwenyekiti wa mtaa wameamua kutuita wachochezi sisi tusioelewa mradi huu kwa kuwaomba stahiki zetu za kisheria kama kupata aridhi mbadala ambacho cha msingi. kumekuwa na tabia ya kulihusisha jeshi la polisi katika hili ,ambayo si sahihi ,kimsingi kuna tabaka mbili kati ya wale wanajua thamani ya mali zao na ugumu wa upatikanaji na wale wasiojua thamani ya mali zao na upatikanaji kwa kuwa wamerithi,ili kutuweka pamoja tunakuomba uje uitishe mkutano kibada mtaa wa kifurukwe na uvumba utusaidie . jitahidi sana kupokea simu zetu kwani tunamatatizo makubwa, sisi tusioelewa mradi tumetengwa na viongozi wa eneo letu.
    nashukuru sana kwa kupata fursa hii.

    Like

  11. Kasim Magae says:

    Kasim Magae says: Hongera Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri inayotoa mfano kwa wengine. Wakazi wote wa kigamboni tunaunga mkono jitihada zako za kusimamia na kututetea sisi wanyonge kutoka kwa wenye tamaa na mali za watu wengine. Mungu akubariki sana.

    Like

  12. Mohammed Sheya says:

    Natoa shukran zangu za dhati kwa taarifa hii iliyoandaliwa na mbunge wetu Dkt Ndugulile. Nakubaliana na hoja zilizotolewa humo na mapendekezo ya kikao kilichofannyika na Waziri Mkuu. Nakubaliana na Mhe Mbunge na wadau wengine kuwa mradi huu umetawaliwa na usiri mwingi na mapungufu makubwa ya ushirikishwaji wa wananchi. Jukumu kubwa la serikali liwe ni kutoa taarifa sahihi kwa wananchi, kuwashirikisha katika mchakato wa mradi huu na kuwawezesha ili wayafikie maendeleo ya kijamii na ya kiuchumi. Ardhi ndio rasilimali ya mwananchi. Matumizi sahihi ya ardhi yatamuondoa mwananchi kwenye umasikini. Kwa kumwezesha mwananchi kuendeleza ardhi yake yeye mwenyewe ama kwa kuingia ubia na wawekezaji ndio njia sahihi ya kumwezesha kiuchumi. Sisi wadau wa Kigamboni tunachohitaji ni kuwezeshwa ili tufikie azma hii. Tutashirikiana na mbunge wetu na viongozi wetu ili kutekeleza azma hii. Tunahitaji uwazi, ushirikishwaji na kuwezeshwa.

    Like

  13. Kaliku says:

    Hongera Faustine, japo nimechelewa kuisoma hii taarifa yako ila inatia moyo kuwa unasimama na wananchi unaowawakilisha. Hilo linapendeza sana. Nakutia moyo kuwa jasiri katika jambo hili maana ni mradi mkubwa sana. kuna uwezekano kabisa uchaguzi ujao ukawekewa zengwe wakasema huyu si mwenzetu ni vema ukajipanga kabisaaa ukiona zengwe unaswitch alternative. Kazi ni uwakilishi vyama ni milango tu ya kuingilia kazini

    Like

  14. njigane says:

    huu mradi huko kigamboni unaanzia wapi na unaishia wapi jamani? maana kigamboni ni kubwa naomba ufafanuzi

    Like

Leave a comment